Friday, January 22, 2016

FAHAMU KUHUSU SAUTI YA MUNGU KWAKO.


FAHAMU NAMNA YA KUSIKIA NA KUIELEWA SAUTI YA MUNGU ILI IKUSAIDE KATIKA KUFANYA MAAMUZI.



Lengo kuu la somo hili ni kumsaidia Mwanadamu yeyote yule aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu kujua namna anavyoweza kusikia Sauti ya Mungu na Kuielewa Sauti ya Mungu. Kwanini? Kwasababu ni wachache sana wanao sikia na kuilewa sauti ya Mungu pamoja na kuwa Mungu huzungumza nao mara kwa mara. Wengine hujiuliza swali hili; Je ni kweli Mungu anazungumza na mwanadamu hata sasa? Hili ni moja ya swali ambalo watu wengi wamekuwa wakijiuliza na kukosa majibu muafaka kwani baadhi yao hawaamini kwamba ni kawaida ya Mungu kuzungumza na wanadamu. Kama ilivyokuwa katika agano la kale, agano jipya, naam hata sasa, Mungu ni yeye yule jana na leo na hata milele.

Maandiko yanadhibitisha wazi kuwa ni kweli Mungu anazungumza na mwanadamu hata hivi leo na si Mitume na Manabii tu tunaowasoma katika Biblia, lakini hata mimi na wewe katika ukawaida wetu Mungu husema nasi.



Mungu anasema “Enyi watu, nawaita ninyi; Na sauti yangu ni kwa wanadamu” (Mithali 8:4). Hivyo ni kusudio la somo hili kuongeza ufahamu wako ili uweze kujua ni kwa namna gani Mungu huzungumza na mwanadamu na kisha nini ufanye ili kumuelewa Mungu anapozungumza na wewe. Ni muhimu kwanza tujiulize swali hili muhimu tunapotafakari somo hili, Kwa nini Mungu azungumze/aseme na mwanadamu? Jibu la swali hili, linalenga kutaka kujua sababu za Mungu kuzungumza na mwanadamu au mwanadamu anahitaji kuisikia sauti ya Mungu ili:-

       I.            Aishi sawasawa na kusudi au mapenzi ya Mungu awapo hapa duniani. Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; Nitakushauri, jicho langu likikutazama. (Zaburi 32:8)

   II.            kujenga na kudumisha mahusiano/mawasiliano mazuri kati yake na Mungu. Kutoka 33:11 Naye Bwana akasema na Musa uso kwa uso, kama vile mtu asemavyo na rafiki yake. Kisha akageuka akarejea hata maragoni; bali mtumishi wake Yoshua, mwana wa Nuni, naye ni kijana, hakutoka mle hemani

III.            kuona kama Mungu aonavyo na hivyo kutafsiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Yeremia 1:11-12 “Tena neno la Bwana likanijia, kusema, Yeremia, waona nini? Nikasema, Naona ufito wa mlozi. Ndipo Bwana akaniambia, Umeona vema, kwa maana ninaliangalia neno langu, ili nilitimize.



MAMBO MHUMU YA KUJUA KUHUSU SAUTI YA MUNGU

Yafuatayo ni baadhi ya mambo muhimu ya kukusaidia kuijua, kuisikia na kuielewa sauti ya Mungu, nawe hunabudi kuyafahamu na kuyatenda:-

1.     Jenga na kudumisha mahusiano mazuri na Roho Mtakatifu – Ni vizuri ukafahamu kwamba Roho Mtakatifu yupo duniani sasa akiliongoza kanisa katika kuyatenda mapenzi ya Mungu. Hivyo uwepo wa mahusiano mazuri kati yako na Roho Mtakatifu ndio ufunguo wa mawasilaino mazuri kati yako na Mungu. Biblia inasema wazi kabisa katika 1Wakorinto 2:10

Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu… vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu”. Andiko hili linatuonyesha umuhimu na nafasi ya Roho Mtakatifu katika kutusaidia kuisikia sauti ya Mungu. Hivyo jenga na kudumisha uhusiano wako na yeye, itakusaidia sana katika kiujua na kuisikia sauti ya Mungu.



2.     Ongeza ufahamu wa viashiria (signal) vya mawasiliano kati yako na Mungu Ufahamu wa viashiria (signal) za mawasiliano kati yako na Mungu ni wa lazima ili kusikia na kuielewa sauti ya Mungu. Zipo alama mbalimbali kwa kila mwamini ambazo Mungu hutumia katika kusema naye. Biblia katika 1Samweli 3:9 inasema “… Enenda, kalale, itakauwa AKIKUITA, utasema, Nena, BWANA; kwa kuwa mtumishi wako anasikia…” Kwahiyo kiashiria kimojawapo ambacho Mungu anakitumia kusema na Mwanadamu ni KUITA, naam anaweza kukuita kwa sauti itokayo kinywani pake au KWA NJIA KUKULETEA ALAMA/VIASHIRIA VYENYE KUKUFANYA UJUE MUNGU ANANIITA.



Kama ilivyo kwa jinsi ya kibinadamu anayekuita si lazima aongee, anaweza kutumia alama za mikono au hata maandishi nk, kukuita. Katika kukuita kwa njia ya viashiria/alama Mungu anaweza kuleta nguvu/msisimuko/ubaridi/maumivu fulani kwenye sehemu ya mwili wako au huzuni moyoni mwako kama ishara/kiashiria cha uwepo wake juu yako na hivyo KUTAFUTA/KUTAKA USIKIVU WAKO ILI ASEME NAWE. Hivyo ni lazima uwe na ufahamu na utafute kujua kuhusu alama/namna ya kwako ambayo Mungu hutumia kutafuta usikivu wako.



N: B Tambua kuwa Ipo namna ya kwako ambayo Mungu hupenda kusema na wewe ambayo inaweza kabisa ikawa tofauti na anavyosema na rafiki yako, Mke, Mume au ndugu yako. Ni jukumu lako kujua viashiria hivyo kwa upande wako kwa kumuuliza Roho Mtakatifu pekee ambae hutufunulia siri za Mungu. Usijefanya vitu kwa Mkumbo au kuiga kutoka kwa rafiki yako na ikakugharimu.



3.     Ni lazima ujue kutofautisha sauti ya Mungu na sauti nyingine. Hapa ndipo penye mtihani mkubwa sana kwa watu wengi mno, kama ilivyokua kwangu kabla sijajifunza kuhusu jambo hili. Ni muhimu sana kwako kulielewa ili usije ukaipuuza sauti ya Mungu kwa kudhani ni mawazo yako au ni ya Shetani au usije ukatekeleza jambo ukiamini kwamba Mungu amesema nawe kumbe Shetani ndiye alisema nawe. Shida ya namna hii aliipata Samweli wakati huo akiwa mtoto na Mungu alikusudia kumuita kwaajili ya Taifa la Israeli. Mungu alimuita kwa sauti yake lakini hakuitambua, badala yake alifananisha na sauti ya Babu yake Mzee Eli. Maandiko yanasema “Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona), na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu; basi, wakati huo Bwana akamwita Samweli; naye akasema, Mimi hapa. Akamwendea Eli kwa haraka, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akasema, Sikukuita; kalale tena. Naye akaenda, akalala tena. Bwana akaita mara ya pili, Samweli! Samweli! Akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akajibu, Sikukuita, mwanangu; kalale tena. Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto. Kwa hivyo Eli akamwambia Samweli, Enenda, kalale; itakuwa, akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Basi Samweli akaenda akalala mahali pake. Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia (1Samweli 3:2-10). Ni muhimu ukaelewa kwamba Mungu anaweza kusema na wewe hata kama uko katikati ya mkutano wa watu wenye kelele nyingi sana. Hii ni kwa sababu Mungu hatumii mdomo kusema nasi bali anatumia moyo wako kuzungumza. Moyo ndio kiungo muhimu cha mawasiliano kati ya mtu na Mungu.



Ukisoma katika Matendo ya Mitume 12:22 Biblia inasema “Watu wakapiga kelele, wakasema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya Mwanadamu. Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho”. Kauli hii ya watu ilikuja baada ya Mfalme Herode kuhutubia watu na kutoa maneno makuu. Watu waliamini kwamba ile ilikuwa sauti ya Mungu, kumbe sivyo na matokeo yake Herode alipigwa na Mungu akafa.



Katika hili nataka nikupe Tahadhari ndugu mpendwa, kuna wakati mtu/watu au watumishi wanaweza kunena mambo makubwa na watu wakadhani Mungu wa kweli anasema ndani yao, kumbe ni mungu wa dunia hii. Na ndio maana ni muhimu sana wewe binafsi uongeze ufahamu wako katika kuijua, kuisikia na kuielewa sauti ya Mungu, ili hata mwanadamu akinena unajua kwamba hili limetoka kwa Mungu wa kweli au vinginevyo.



Naam! mpendwa zipo sauti mbalimbali ambazo zote zinalenga kupambana/kuharibu kusudi la Mungu ndani ya mtu, zipo sauti za wanadamu (wazazi, walezi, mwenza wa ndoa, viongozi wa kiroho), ipo sauti ya Shetani kupitia majeshi ya pepo wabaya nk. Ni lazima mwanadamu amjue sana Mungu kiasi cha kutosha ili kuweza kutofautisha sauti hizi. Njia au namna pekee ya kutofautisha sauti hizi na ile ya Mungu ni kuwa na uelewa au ufahamu mkubwa wa Neno la Mungu pekee, kwasababu Mungu hawezi hata siku moja kukuagiza jambo lililo kinyume na Neno lake.



FAHAMU VIKWAZO VINAVYOWEZA KUPELEKEA KUTOKUSIKIA SAUTI YA MUNGU.

Biblia imeainisha vikwazo kadhaa vyenye kupelekea mtu kutokuisika sauti ya Mungu. Nitakuonyesha vikwazo 2 vikubwa na nikupe changamoto ya kuingia ndani Kiimandiko ili kujua vikwazo vyengine:-

       I.            Dhambi au kuishi maisha ya dhambi. Mungu hapendezwi na Mtu anayeishi katika mazingira au maisha ya dhambi, (1Yohana 3:4) “Kila atendaye dhambi, afanya uasi; kwa kuwa dhambi ni uasi”. Maana yake ni kuwa atendaye dhambi anakua amemuasi Mungu, kwahiyo amekwenda kinyume na sheria iliyowekwa na Mungu. Matokeo yake mtu huyo na Mungu wanakua mbali kila mmoja akiacha kujishughulisha na mwenzie. Isaya 59: 1-2 Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia”. Angalia lilee neno ‘HATA HATAKI KUSIKIA’.



    II.            Kukosa uaminifu. (Hesabu 12:7-8,). Mungu hupendezwa sana na Mtu aliye mwaminifu kwake siku zote za maisha yake. Kwa mtu huyo Mungu hujenga mahusiano ya karibu kwa haraka mno na hata kusemezana nae Zaidi. Maandiko yanalidhibitisha hili pale Mungu aliposema mwenyewe akiwaambia Haruni na Miriamu Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. Kisha akawaambia,Sikizeni basi maneno yangu;Akiwapo nabii kati yenu,Mimi,Bwana,nitajifunua kwake katika maono,Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? (Hesabu 12:5- 8). Uhusiano wa karibu sana aliokua nao Musa na Mungu ulitokana na UAMINIFU aliokua nao Musa mbele za Mungu. Mungu alimpenda na kuamua kuingilia kati kwa yeyote yule aliyejaribu kufuatilia au kugusa maisha ya Musa, hakika ni kama alikua akigusa maisha ya Mungu kwasababu haukunyamaza hata kidogo. Cheki kilichomtokea Miriamu baada ya kumsemasema Musa kwa habari ya Mke wake “Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake. Kisha hilo wingu likaondoka kutoka pale juu ya hema; na tazama, Miriamu akawa mwenye ukoma, mweupe kama theluji; Haruni akamwangalia Miriamu, na tazama, yu mwenye ukoma. Kisha Haruni akamwambia Musa, Ee bwana wangu nakusihi sana usituwekee dhambi juu yetu, kwa kuwa tumefanya ya upumbavu, na kufanya dhambi. (Hesabu 12:9-10). Kwa muda wako unaweza soma habari za Samweli katika ile 1Samweli 2:26-35 utajifunza kitu kuhusu uaminifu kupitia wito wa Samweli.

Ipo mifano ya wanamapinduzi wengi amabo walifanya mambo makubwa wakiongozwa na sauti ya Mungu katika kila jambo; akina Daniel, Paulo, Samweli, Yoshua na wengine wengi. Maisha ya uaminifu mbele za Mungu ndiyo ilikua silaha kubwa ya mafanikio na ushindi wao dhidi ya wengine.



MAMBO YATAKAYOWEZA KUKUSAIDIA KUJUA NA KUISIKIA SAUTI YA MUNGU KATIKA MAISHA YAKO.



       I.            Unahitaji kufahamu umuhimu wa Mungu kuzungumza/kusema nawe. Zipo sababu nyingi za Mungu kuzungumza na wanadamu laikini kubwa yenye kuzibeba zote ni ile iliyoandikwa katika Zaburi 32:8 kwamba Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; Nitakushauri, jicho langu likikutazama”. Kwanini? Kwasababu mwanadamu haishi duniani kwa muda ambao Mungu amemuweka kwa kusudi lake mwenyewe, bali ni kwa kusudi la Mungu pekee.

Ndivyo maandiko yanavyotueleza ukisoma kitabu cha (Warumi 8:28)Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Kwahiyo ili uweze kulitumikia vizuri kusudi la Mungu katika maisha yako sharti ni kwamba; lazima uongozwe nay eye katika njia sahihi. Na njia mojawapo ni ya Mungu kusema na wewe. Lengo lake katika kusema na wewe ni kukuongoza katika njia sahihi kwa kukuondoa kwenye makusudi ambayo yapo nje na mapenzi yake kwenye maisha yako maana imeandikwa “Kwa kuwa Mungu hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali. Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani; Ndipo huyafunua masikio ya watu, Na kuyatia muhuri mafundisho yao,Ili amwondoe mtu katika makusudio yake, Na kumfichia mtu kiburi; Yeye huizuia nafsi yake isiende shimoni, Na uhai wake usiangamie kwa upanga” (Ayubu 33:14-18)



    II.       Ongeza ufahamu wako kuhusu ulimwengu wa roho. Mambo yote yanayotokea katika ulimwengu wa mwili yameanzia katika uilimwengu wa roho, naam maamuzi ya kile ambacho hutokea katika ulimwengu wa mwili hufanyika katika ulimwengu wa roho. Zaidi hata mapambano (vita vya kiroho) yote aliyoanayo mwanadamu katika kulitumikia kusudi la Mungu hufanyika katika ulimwengu wa roho.

Hivyo kuwa na ufahamu wa ulimwengu wa roho hususani namna ya kuishi na kuwasiliana katika ulimwengu huo ni muhimu sana kwa mwamini mwenye kutafuta kujua na kuisikia sauti/mawazo ya Mungu katika maisha yake. Kwa kuwa Mungu ni roho kama alivyo na Shetani pia. Hebu tusome habari ya Elisha na Mtumishi wake, 2 Wafalme 6:8-17. Maandiko yanatueleza kwamba Shetani nae ni roho ukisoma Waefeso 6:10-12.



Ndugu mpendwa usiruhusu yale unayoyapitia au yale ambayo watu /mazingira yanasema juu yako yabadilishe au kuongoza maisha yako, bali tafuta kuijua na kuielewa sauti ya Mungu kwenye maisha yako. Na ndiyo maana somo hili limekuja ili kukusaidia kufika mahala ambapo utaweza kuyatenda mapenzi kamili ya Mungu kwenye maisha yako.






Share:

USCF-SJUT NEWS

Designed by Joel Elphas @ 2015. Powered by Blogger.

Recent Posts