Saturday, January 23, 2016

JIFUNZE BIBLIA INASEMAJE KUHUSU ADHARI NA MATOKEO YA KUFANYA DHAMBI YA UZINZI/UASHERATI KWA MTU ALIYEOKOKA.


ADHARI NA MATOKEO YA DHAMBI YA  UZINZI/UASHERATI KWA MTU ALIYEOKOKA.

Katika Mithali 6:32 Biblia inasema “Mtu aziniye na mwanamke hana akili kabisa; afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake” na pia katika  Mithali 6:26 inasema “Maana kwa Malaya mtu hutiwa katika hali ya kuhitaji kipande cha mkate; na kahaba humwinda mtu anase nafsi yake iliyo ya thamani”



UZIZI/UASHERATI: Ni tendo la ndoa linalofanywa na mtu mume na mtu mke kinyume na mapenzi ya Mungu/ kabla ya wakati sahihi wa Mungu (Ndoa takatifu).



Ni watu wengi sana ambao wamerudi nyuma na kuanguka katika dhambi hii. Hadi sasa bado kuna kundi kubwa la watu waliokoka ambao bado dhambi hii ina nguvu juu yao na bado wanafanya jambo hili kinyume na mapenzi ya Mungu katika maisha yao.



Si kana kwamba Mungu anafuga dhambi kwa kutokuwadhihirisha hao watu na uovu wao, isipokuwa hataki jina lake litukanwe, kwa kuwa ikijulikana huyo mtu au hao watu wameanguka huenda  kutokana na nafasi zao kiuongozi, kihuduma kiushuhuda nk jina la Mungu litatukanwa sana na mataifa lakini pia hata na wale waliokwisha kuokoka. Kwa lugha rahisi hao watu au huyo mtu atakuwa ametoa nafasi ya jina la Mungu kutukanwa.



Kwa bahati mbaya sehemu kubwa ya watumishi wa Mungu katika makanisa yao hawaoni athari ya hili jambo katika upana wake kama Biblia inavyosema.   Inafika mahali baadhi yao wanawafariji wale walioanguka kwa kusema jipe moyo, tubu na Mungu ni wa rehema atakusamehe. Na wengine utasikia wanasema haukuanza wewe, Daudi naye yalimshinda sembuse wewe!!.



Wengine wanatumia maandiko kabisa wanasema ‘mwenye haki huanguka mara saba’ we mara moja tu wala isikusumbue sana tengeneza tu Mungu atakusamehe, na wengine wanasema mimi mwenyewe nilishindwa kwahiyo, hata wewe isikusumbue saana kazana tu uoe wa kwako au omba upate mume/mke. Ni kama vile watu wanatumia rehema/neema ya Mungu kuendelea kutenda dhambi tena kwa ujasiri.



Sikiliza, si kana kwamba napingana na neno au na mawzo ya hao watumishi wenzangu La hasha!. Nakubali kwamba Mungu husamehe dhambi na maovu  ikiwa ni pamoja na dhambi hii ya uasherati/uzinzi (Matendo ya Mitume 3:19 ‘Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana’).



LAKINI TAMBUA Mungu husamehe kwa sababu 2 kubwa sana:-

Ø  Moja hafurahii kifo cha mwenye dhambi ‘Ina thamani machoni pa Bwana mauti ya wacha Mungu wake’ Zaburi 116:15.

Ø  Na pili ni ili kukurejesha kwenye nafasi yako ili uweze kulitumikia kusudi lake.

Lakini je, unajua madhara/matokeo ya dhambi hii kwa mtu aliyeokoka anapoifanya? Hata kama Mungu akikusamehe/amekusamehe, unajua nini kimetokea/kilitokea kwako pale ulipofanya dhambi hii? Au je unaijua gharama ya kurejea kwenye nafasi yako aliyoikusudia Mungu?





Biblia inasema aziniye na mwanamke afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake? Huenda huwa unausoma tu huo msitari bila kujua uzito wa hayo maneno. Ni vizuri kwanza ukajua kwamba ndani ya nafsi ya mtu ndiko kwenye hisia, nia (utashi), akili, na maamuzi. KUBWA Zaidi kwa Mungu nafsi ndiyo ‘operating system’ kama kwenye computer, kwa maana ndiyo kiwanda kinachotoa tafsiri ya kila kitu ambacho Mungu anazungumza/sema na mwanadamu



MAMBO 3 YANAYOTOKEA MTU ALIYEOKOKA ANPOFANYA DHAMBI HII YA UASHERATI/ZINAA:-



1.   Kuharibika kwa mfumo wa mahusiano na mawasiliano kati yake na Mungu.



Katika  mfumo wa ufalme wa Ki – Mungu ni kawaida kwa mtu aliyeokoka na mwenye mahusiano mazuri na Mungu, kuona Mungu akiwasiliana/akisema naye kwa njia mbalimbali ili kumshirikisha mawazo na mipango yake ikiwa ni namna ya kumuongoza mtu huyo katika kusudi lake chini ya jua.  Hii ina maana suala la mawasiliano kati ya mtu na Mungu ni la kawaida kwa mtu mwenye mahusiano mazuri na Mungu wake.



Sasa mtu anapofanya dhambi hii, athari yake ni hii, dhambi inaharibu mfumo huu wa mahusiano kati ya mtu na Mungu. Na mahusiano kati ya mtu na Mungu yakiharibika mawasilano kati ya Mungu na mtu yanakatika/kuharibika pia. Ninaposema yanakatika ina maana si rahisi kwa Mungu kusema tena na huyo mtu au huyo mtu kusema tena na Mungu wake kwa sababu asili/mazingira hayaruhusu na hili linapelekea mafunuo/sauti ya Bwana kuwa hadimu kwako, kwa kanisa, kwa jamii, kwa kampuni na hata nchi tegemeana na nafasi yako katika ufalme wa Mungu.

2.   Kuharibika kwa mfumo wa kufanya maamuzi/kufikiri ndani yako.

Dhambi hii inaharibu mfumo wa kufanya maamuzi, shetani anapomuongoza mtu kufanya dhambi hii, lengo/interest yake ipo kwenye nafsi ya mtu huyo. Shetani akikamata nafsi ya mtu maana yake amekamata akili/nia ya mtu huyo, akikamata akili ya mtu huyo maana yake amekamata maamuzi yake pia. Na akikamata maamuzi yako amekamata matokeo ya maisha yako ya sasa na ya baadae.



Hivyo mtu huyu hataweza tena kufikiri mambo ya rohoni kama Paulo anavyoagiza kwa Warumi ile sura ya 8:5Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili, bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho”. Hivyo kufanya dhambi hii ni kuathiri mfumo wako wa kufanya maamuzi, na hii ina maana hata Mungu akileta wazo lake kwako huwezi kulipokea maana mfumo wa kuamua umeukabidhi kwa Shetani kwa njia ya zinaa/uasherati.



3.   Kuharibika kwa mfumo wa utiifu ndani yako.



Warumi 2:13 ‘Kwa sababu sio wale wasikiao sheria walio  wenye kuhesabiwa haki, bali ni wale waitendao sheria watakaohesabiwa haki”. Baada ya matokeo hayo 2 hapo juu hiki ndicho kinachozaliwa mwishoni. Ubaya wa dhambi hii inaharibu mifumo hii ambaayo ndiyo misingi ya mwenye haki. Fuatili maisha ya watu wengi sana walioanguka kwenye dhambi hii angalia utiifu wao mbele za Mungu ukoje. Nakuhakikishia utagundua ni ngumu sana kwao kutii maagizo ya Mungu kwao. Mtu wa aina hii hata Mungu akimpa maagizo ya kutekeleza hataweza kwa kuwa tayari mahusiano yamevunjika, mamuzi yametekwa .



JE MUNGU ANATAKA TUJIFUNZE NINI KUPITIA HILI? 



Unapokuwa na mahusiano mazuri na Mungu  hii mifumo yote mitatu/Mambo yote 3 yatafanya kazi vizuri na ndiyo kusudi la Mungu. Dhambi hii inapoingia inasababisha kuharibka kwa mifumo hii mitatu (MAHUSIANO,KUFIKIRI NA UTII). Kitu kibaya au kinacho muumiza Mungu ni kwamba hata kama akikusamehe pale utakapotubu, LAKINI itakugharimu sana kuirejesha mahali pake mifumo hii 3. Na ndio maana neno linasema afanya jambo litakalomwangamiza nafsi yake, kwahiyo utakua unakazi ya kurejesha NAFSI yako katika upya wake na ni garama sana sana tu. Kwasababu kila kilichomo ndani ya nafsi (HISIA, NIA, AKILI, MAAMUZI) kimeangamizwa. Ili kuirejesha mifumo hii maombi ya muda mrefu ya rehema na kutengeza mahali palipobomoka ni ya lazima.  



PENGINE unaweza kusema la muhimu Mungu amenisamehe, hayo mengine sijali sana. Unaweza kusema hayo maneno kama hujui/ huelewi muda unathamani kiasi gani kwa Mungu, na pia mahusiano kati ya muda na Mungu.



NGOJA NIKUAMBIE SIRI YA MUNGU NA MUDA JAPO KIDOGO; Muda na Mungu ni marafiki, na tena wote wana mahusiano mzuri sana.  Muda anaongoza maamuzi ya Mungu na Mungu anaongoza matumizi ya muda kwa kuiweka mipango ndani ya mtu na kumwagiza atekeleze ndani ya muda. Hivyo kwa Mungu muda ni muhimu sana.



Kitu gani namaanisha hapa; Mungu hakutenga/kuweka muda wa mtu kurejesha mifumo hii kwa sababu umeanguka katika dhambi. Katika kipindi ambacho wewe unatubu na kutengeneza kwa Mungu wako ili kurejesha mifumo hii, basi uwe na uhakika upande wa pili umesha athiri kusudi la Mungu duniani kupitia wewe ambalo limefungwa katika muda. Sasa kama utatumia siku tano, mwezi mmoja, miezi sita, mwaka mzima nk, kurejesha hii mifumo basi kwa kipindi hicho chote utakuwa umekwamisha kusudi la Mungu kupitia wewe. Na ndio maana Biblia inasema Shetani anawinda nafsi yako iliyo ya thamani, maana anajua akikamata nafsi yako amekamata akili, nia, hisia na maamuzi yako na hivyo amefanikiwa kuharibu hiyo mifumo na kusababisha mipango ya Mungu isifanyike kwa muda aliokusudia kupitia wewe.



Kwa Mfano; Fikiria umepangiwa na Mungu kusafiri umbali wa kilomita 500 ndani ya masaa saba (7).  Mungu amekupa gari ambalo ni kusudi lake  kwako. Hivyo litazame gari ulilopewa kama kusudi la Mungu kwako na wewe ni dereva. Sasa wewe ukaamua kuliendesha  gari bila kuweka maji kwenye injini. Baada ya kusafiri umbali wa kilomita 300 injini ya gari ikafa kwa kukosa maji na mbele yako zimebaki kilomita 200. Je unajua utakuwa umeathiri kwa kiwango gani kusudi la Mungu? Kutokana na mfano huu, unapotenda dhambi hii  je unajua ni kwa kiwango gani utakuwa umeathiri mipango ya Mungu kupitia wewe duniani kwa kipindi chote ambacho utakuwa unairejesha mifumo iliyopo ndani ya nafsi yako mahali pake?.



Kinacho muumiza/huzunisha Mungu kimsingi si kwa sababu umeanguka dhambini, lakini ni kwa sababu kuanguka kwako dhambini kunamzuia yeye kukutumia wewe mpaka hiyo mifumo yote irejee mahali pake. Hii ina maana interest ya Mungu ipo kwenye muda. Maana anajua itakugharimu wewe muda wa kutengeneza na itamgharimu yeye muda wa kukusubiri wewe utenegeze mifumo hii.



Mpendwa kumbuka hili usije sahau, Mungu hategemei wewe uanguke katika dhambi hii, maana kadri unavyoanguka ndivyo unavyokwamisha na kuchelewesha kazi ya Mungu duniani kupittia wewe. Je unajua hasara na matokeo ya kukwamisha na kuchelewesha kazi ya Mungu?



Je katika nafasi ambayo Mungu amekupa Kazini, huduma, au kanisa unachunga kwa kiasi gani nafsi yako isiharibiwe na dhambi hii? Neno linasema Matendo ya Mitume 20:28Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe”.

Naamini ujumbe huu utakusaidia kuhakiksha unafanya maamuzi ya kutofanya tena dhambi hii si kwa sababu imeandikwa tu usizini bali ni kwa sababu unampenda Mungu na unataka kuhakikisha kusudi la Mungu linafanikiwa bila kukwamishwa kwa dhambi hii.



                                                   Mwisho.

                            ******** MUNGU ATUSAIDIE. *********


Share:

USCF-SJUT NEWS

Designed by Joel Elphas @ 2015. Powered by Blogger.

Recent Posts